MAMBO USIYO YAJUA KUMUHUSU BOB MARLEY

chuwaz.com


Filamu mpya, One Love, inaadhimisha maisha na kazi ya mwanamuziki nguli wa reggae wa Jamaica, Bob Marley.

Filamu hiyo inaeleza safari ya mwanamuziki huyo kutoka utotoni mwake hadi umaarufu mkubwa na inaangazia hadithi na matukio yanayojulikana sana.

Lakini kuna mambo mengi kuhusu msanii huyu ambayo hayajulikani. Haya hapa ni mambo manne ambayo huenda hukuyafahamu kuhusu nyota huyo wa reggae.

1. Nyota wa J-Reggae

Je wajua kwamba Bob Marley alisaidia kutangaza reggae nchini Japan?

Mnamo mwaka 1975, Marley alizuru Japan. Kulingana na Jarida la japan la Sabukaru, Masahito “mwimbaji huyo alikua na mpiga ngoma maarufu Masahito "Pecker" Hashida.

Hii ilisababisha ushirikiano wa muziki kwenye albamu mbili zenye ushawishi - Pecker Power mwaka wa 1980 (akimshirikisha Marley) na Instant Rasta 1981, zote zilirekodiwa katika Studio za Channel One huko Jamaica.

Albamu hizo ziliangazia wasanii wa Jamaica na Japan na zilichukua jukumu muhimu katika kueneza umaarufu wa reggae nchini Japan.

Reggae ni maarufu nchini Japan hadi leo na inaadhimishwa katika matukio kama vile tamasha maarufu la reggae la Yokohama au Yokohama Reggae Sai, ambalo hufanyika kila majira ya joto kati ya Julai na Septemba.

2. Mshindi wa Tuzo ya Umoja wa Mataifa

Marley anajulikana sana kwa nyimbo zake za kijamii na kisiasa.

Lakini je, unajua kwamba mwaka 1978, alitunukiwa nishani ya amani na Umoja wa Mataifa?

Hii ilikuwa kwa ajili ya kazi ya mwimbaji huyo katika kukuza amani na haki wakati wa machafuko ya kisiasa nchini Jamaica.

Mapema mwaka huo, Marley alikuwa ametumbuiza katika Tamasha la Amani la One Love huko Kingston, Jamaica.

Tamasha hilo lililenga kupunguza ghasia za magenge ya kidini na Marley alikuwa amewaleta pamoja wapinzani wa kisiasa kupeana mikono jukwaani.

Tuzo hilo la Umoja wa Mataifa lilitolewa kwa mwimbaji huyo miezi michache baadaye katika ukumbi wa Waldorf Astoria mjini New York, uliowasilishwa na wajumbe wa Afrika kwenye Umoja wa Mataifa.

3. Mtabiri

Kabla ya kuwa mwanamuziki, Bob Marley alikuwa msomaji viganja katika mji aliozaliwa wa St Ann huko Jamaica.

Akiwa mtoto, alisoma viganja vya marafiki na majirani ili kuwaambia yale yatakayotokea wakati ujao.

Kulingana na rafiki wa karibu wa mwimbaji na msiri, Allan "Skill" Cole, utabiri mwingi wa Marley ulikuwa na kiwango cha usahihi.

Lakini Cole, ambaye alisimamia ziara za tamasha za Marley katika miaka ya 1970, pia alisema mazoezi ya kusoma viganja yalipingwa nchini Jamaica wakati huo.

Jumuiya ya Rastafary karibu na Marley ilimhimiza kuacha kusoma viganja.

Marley alikubali, lakini si kabla ya kutabiri kwa usahihi kwamba siku moja angejenga studio yake.

4. Mfanyakazi wa kiwanda cha Chrysler

Alipokuwa akijitahidi kujikimu kimaisha kama mwanamuziki, Marley alifanya kazi kwa muda mfupi katika kiwanda cha magari cha Chrysler katika jimbo la Delaware nchini Marekani.

Mnamo 1966, licha ya vibao vichache vya Ska huko Jamaica, Marley bado hakuwa amepata umaarufu wake katika tasnia ya muziki.

Kwa hivyo aliondoka nchi yake kwenda Wilmington, Delaware ambapo mama yake, Cedella Booker, alikuwa akiishi tangu kifo cha baba yake Marley mnamo 1955.

Kulingana na marafiki, kazi ya mwisho ilihimiza wimbo wake wa Night Shift, ambao ulijumuishwa katika albamu yake ya 1976 ya Rastaman Vibration.

Chanzo 

BBC Swahili


Previous Post Next Post

No Thumbnail

News app yako bomba sasa unaweza idownload kwa kubonyeza batani ya download hapa ,